Advertisements

Sunday, January 21, 2018

Polepole awaza CCM bila upinzani

Katibu  wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya Chama cha Mapinduzi (CCM), Itikadi na Uenezi, Humphrey Polepole, amesema kama chama hicho kitajipanga vizuri zaidi na kutekeleza majukumu yake kama inavyotakiwa, hakutakuwa na upinzani.

Polepole aliyasema hayo juzi, wakati akiwapokea viongozi kadhaa waliovihama vyama vyao na kujiunga na CCM wakitokea mikoa ya Dodoma, Siginda, Tabora na Kilimanjaro.

"Mimi nawaeleza kama wana CCM tutajipanga vizuri na kuachana na ubinafsi, heshima ya chama chetu mkoani Kilimanjaro itarejea kwa sababu tutakapotekeleza majukumu yetu inavyotakiwa, upinzani hautakuwapo," alisema.

Viongozi hao 37 kutoka Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) na ACT-Wazalendo walijiunga na CCM na kupokewa na Polepole katika ofisi za chama hicho Mkoa wa Kilimanjaro mjini hapa.


Kwa mujibu wa Polepole, chanzo cha kuhama kwa baadhi ya wanachama wa CCM mwaka 2015 na kwenda upinzani, kilikuwa ukiukwaji wa misingi ya haki na wajibu ndani ya chama hicho.

"Msingi ya kuanzishwa kwa CCM ni kusimamia haki na wajibu wa watu, hivyo kuhama kwa wanachama hao kulitokana na kukosekana kwa haki na CCM kukosa mvuto kwa watu. Lakini sasa tumetambua ni wapi tumekosea ndiyo maana CCM ya sasa imekuwa na mvuto,” alisema.

Aliongeza kuwa: "Kwasasa walioihama CCM wameanza kurejea Kutokana na chama sasa kurejesha imani, haki na wajibu kwa wanachama.”

Alisema CCM ya sasa imejenga imani kubwa kwa Watanzania kutokana na kufanyika kwa uboreshaji na utendaji kazi wa Mwenyekiti waTaifa CCM, Rais Dk. John Magufuli.

Polepole alisisitiza kwamba mageuzi makubwa yanayofanyika kwa sasa ndani ya chama hicho yamerudisha chama mikononi mwa wananchi na kuwataka wana CCM wasiwakatae wanachama wanaotoka upinzani.

Pia aliwataka viongozi wa chama mkoani Kilimanjaro kuhakikisha wanawasimamia watendaji wa serikali kwa karibu ili kuhakikisha wanatimiza majukumu yao kwa mujibu wa sheria ikiwamo kutoa fedha za mikopo kwa vikundi vya wanawake na vijana.

No comments: