Advertisements

Thursday, October 13, 2016

HISTORIA FUPI YA MAREHEMU DIDAS MASABURI

Mwaka 1995, Dk. Masaburi aliwahi kuwa Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) Mkoa wa Dar e Salaam .
Mbali na hilo pia alibahatika kuwa na Shahada ya Juu ya Masuala ya Ugavi iliyotolewa na Bodi ya Uhasibu ya Taifa (NBAA), huku kwa miaka kadhaa akifanikiwa kuwa mfanyakazi wa Kiwanda cha vinywaji cha Chibuku.
Pia amefanyakazi Wizara ya Elimu, Utamaduni na Michezo kupitia mradi maalumu wa Benki ya Dunia (WB) na amekuwa akimiliki Shule ya Sekondari ya Dk. Didas Masaburi iliyopo Mbagala jijini Dar es Salaam pamoja na anamiliki Chuo cha Ugavi na Manunuzi kilichopo Chanika.
Dk. Masaburi alikuwa akiishi na figo moja kwa tangu mwanzoni mwa miaka 2000 hadi mauti yanamkuta.

Safari ya siasa
Mwaka 2015, marehemu Dk. Didas Masaburi, alijitosa katika kunyang’anyiro cha ubunge katika jimbo la Ubungo kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambapo alishindwa na aliyekuwa mgombea wa Chadema, Saed Kubenea ambaye alitangazwa kuwa mbunge hilo kwa kura 87,666 huku Masaburi akipata kura 59,514.
Mwaka 2010, Dk. Masaburi alichanguliwa kuwa Diwaniwa wa Kata ya Kivukoni na Desemba 23, akachaguliwa kwa Meya mpya wa Jiji la Dar es Salaam, kwa kuibuka mshindi katika kinyang’anyiro cha uchaguzi uliofanyika kwenye Ukumbi wa Karimjee jijini Dar es Salaam ambapo aliwashinda wapinzani wake, Diwani wa Kata ya Tandale, Amir Mbunju (CUF).
Meya huyo wa zamani alichaguliwa kwa kura 125 huku wajumbe wanne kati yao hawakupiga kura na 9 ziliharibika.

Kauli tata za kukumbukwa
Agosti 6, mwaka 2011, Dk. Masaburi aliingia katika malumbano ya wabunge wa Mkoa wa Dar es Salaam ambao walimtaka ajiuzulu kutokana na kukiuka taratibu katika uuzwaji wa Shirika la Usafiri Dar es Salaam (UDA).
Kutokana na hali hiyo meya huyo wa zamani alijibu mapigo dhidi ya wabunge hao ambapo alisema baadhi yao wanashindwa kufikiri kwa kutumia vichwa na badala yake wanafikiri kwa kutumia ‘makalio’.
Alisema wabunge katika kuchangia hoja ya suala la UDA wamegawanyika katika mafungu matatu ambao alisema katika mafungu hayo moja halijui lolote kuhusiana na sakata hilo na limedandia tu hoja.
Alitaja kundi la pili kuwa ni la wabunge wa jiji la Dar es Salaam ambao ni Mbunge wa Ubungo wa wakati huo, John Mnyika, na Mbunge wa Kawe, Halima Mdee, ambao alisema wanatafuta umaarufu wa kisiasa kupitia sakata la UDA.
Alisema Mnyika aliweza kuhoji hata katika vikao rasmi, lakini Mdee hajui chochote kwa kuwa hajawahi kuhudhuria vikao vya jiji mpaka sasa.
Aidha, kundi la tatu ambalo ndilo alilituhumu zaidi kufikiri kwa kutumia “makalio” badala ya kichwa ni la wabunge Abasi Mtemvu aliyekuwa (Temeke), Mussa Azzan ‘Zungu'(Ilala) na Dk. Makongoro Mahanga aliyekuwa (Segerea) ambao alidai kuwa wanajua ukweli wa jambo hilo lakini wanapotosha ili kuficha madhambi yao ambayo alisema yataibuliwa muda si mrefu ya ufisadi ndani ya jiji hilo.

Escrow yamuibua
Kutokana na sakata hilo ambalo liliitikisa Serikali ya awamu ya nne chini ya Rais mstaafu Jakaya Kikwete, Dk. Masaburi alijitokeza hadhani baada ya makombora kutoka kwa wabunge na kutaka kiongozi huyo wa nchi kutobebeshwa mzigo huo.
Alisema Rais Kikwete amefanyakazi kubwa ya kuhakikisha anawashughulikia waliohusika hivyo hastahili kuingizwa kwenye kapu hilo.

Tukio la mwisho
Kabla ya kufikiwa na mauti Dk. Masaburi alipelekwa nchini India mara mbili kwa ajili ya matibabu na kwa mara ya mwisho alionekana hadharani Serena Hoteli ambapo alikwenda kutoa mada kuhusu masuala ya manunuzi.
Baada ya kutoa mada akiwa njiani anarejea nyumbani kwake alijisikia vibaya na shinikizo la damu kushuka ambapo alikwenda hospitali kwa matibabu.

No comments: