Advertisements

Tuesday, August 23, 2016

MKE WA MTANZANIA ALIYENG'ARA OLYMPIC AFUNGUKA


WINFRIDA NGONYANI -DAR ES SALAAM NA ELIYA MBONEA, ARUSHA

MKE wa Mtanzania aliyeng’ara katika michuano ya Olimpiki, Alphonce Simbu, Rehema Daudi, amefunguka na kusema kuwa ushindi wa mumewe huyo ambaye anaendesha maisha yake kwa kukimbia umetokana na juhudi zake binafsi na sapoti kubwa aliyoipata kutoka Chama cha Riadha Tanzania (RT).

Rehema mwenye umri wa miaka 22 na mtoto wa miezi nane, ameeleza kuwa anamsubiria kwa hamu mumewe huyo ambaye ameitoa kimasomaso Tanzania baada ya kushika nafasi ya tano katika mashindano ya mbio ndefu kilomita 42 (marathon) yaliyofanyika jijini Rio De Janeiro Brazil, ambapo Mkenya, Eliud Kipchoge, alishinda mbio hizo na kutwaa medali ya dhahabu.

Akizungumza kwa furaha na MTANZANIA jijini Arusha, Rehema ambaye yupo kwenye ndoa na mwanariadha huyo kwa mwaka mmoja na nusu, alisema ushindi mumewe umempa faraja kubwa sana na anamshukuru Mungu kwa juhudi za mumewe.

“Namshukuru Mungu na nina furaha kubwa kwani mume wangu ameweza kututoa kimasomaso Watanzania na familia kwa ujumla, alikuwa na juhudi sana wakati akiwa kambini hata kabla ya kambi, pia Rais wa RT kwa kweli amesaidia sana mume wangu kufikia hatua hii, ninamsubiria kwa hamu.

“Ninawaomba wanariadha wengine nchini wajitahidi na kujipa moyo, ipo siku nao watafika kwenye hatua nzuri za mashindano ya riadha.

“Mume wangu hana kazi nyingine inayomwingizia kipato zaidi ya kukimbia, amekua akifanya mazoezi sana eneo la Sakina na milimani, Mwenyezi Mungu ameona juhudi zake naamini atamfikisha mbali zaidi ya hapa,” alisema Rehema.

Simbu mwenye umri wa miaka 24, ameweka historia kwa taifa kwa kushika nafasi ya tano akitumia muda wa saa 2:11:15 katika mbio ndefu ‘marathon’, akiwaacha wanariadha 155 walioshiriki mbio hizo licha ya kukosa medali lakini ameweza kuweka historia.

Nafasi ya juu kama ya Simbu katika michuano mikubwa, imewahi kushikwa na wanariadha wakongwe, Filbert Bayi na Suleiman Nyambui, miaka ya 80 katika michezo hiyo iliyofanyika jijini Moscow, Urusi.

Akizungumza na MTANZANIA jana, Rais wa Shirikisho la Riadha Tanzania (RT), Antony Mtaka, alisema ushindi wa Simbu ni heshima kubwa kwa taifa.

“Haya ni matokeo ya maandalizi mazuri na muda mrefu kwa wanariadha wetu, Simbu ameonyesha mwanga kwamba mbeleni Tanzania tunayo nafasi ya kupata medali katika michezo ya Olimpiki,” alisema Mtaka.

Simbu aliweka kambi ya miezi sita katika Chuo cha Wakala wa Misitu (FITI) kilichopo Siha, mkoani Kilimanjaro chini ya kocha wake, Francis John, baada ya kufikia viwango vinavyotakiwa na Shirikisho la Dunia la mchezo huo (IAAF).

Kiwango alichofikia mwanariadha huyo kijana ni kukimbia muda wa saa 2:19:00 alipokuwa akipeperusha bendera ya Tanzania katika michezo ya Lake Biwa, iliyofanyika Desemba mwaka jana huko nchini Japan.

Hata hivyo, mwanzoni mwa mwaka huu, Simbu alivunja rekodi yake mwenyewe pale aliposhika nafasi ya 3 katika mashindano hayo hayo kwa kutumia saa 2:09:19 hivyo kufuzu moja kwa moja katika michezo ya Rio mwaka huu.

Dalili za Simbu kufanya vizuri zilianza kuonekana tangu akiwa hapa nyumbani, baada ya kujitosa katika mbio za Bagamoyo Marathon siku chache kabla hajaelekea Rio, ambapo aliweza kushika nafasi ya kwanza.

Katika mbio hizo za Bagamoyo kwa upande wa wanaume kilomita 21, Simbu kutoka Arusha aliibuka mshindi akitumia saa 1:03:56, ambapo kwa asilimia kubwa mbio hizo ziliongozwa na wanariadha wengi kutoka Arusha.

Katika mbio hizo za Bagamoyo, Simbu alikuwa na Mtanzania Saidi Makula aliyeshika nafasi ya nne, ambaye yeye katika Rio 2016 alishika nafasi ya 43 hiyo ikiwa ni baada ya kufikia viwango kwa kukimbia marathon kwa saa 2:13:25 mjini Casablanca, Morocco Oktoba mwaka jana na ndoto yake ilitimia Aprili 3 mwaka huu aliposhiriki marathon ya Daengu, Korea baada ya kukimbia kwa saa 2:12:01.

Wanariadha wengine ambao nao walishiriki katika michezo ya mwaka huu ni pamoja na mwanamke pekee, Sara Ramadhani ambaye alishika nafasi ya 126 na Fabiano Joseph alishika nafasi ya 112.

MTANZANIA

No comments: