Advertisements

Sunday, March 29, 2015

JK: Hakuna mpango wa kuanzisha Mahakama ya Kadhi , Asema mjadala umefungwa

Rais Jakaya Kikwete amefunga rasmi mjadala wa Mahakama ya Kadhi na kwamba hakuna mpango wa kuianzisha.
Rais Kikwete alitoa kauli hiyo jana jijini Dar es Salaam wakati akizungumza na kamati ya amani ya viongozi wa dini mkoa wa Dar es Salaam.

Kauli hiyo ya Kikwete imekuja baada ya hivi karibuni, viongozi dini za Kikristo chini ya Jukwaa la Wakristo Tanzania, kutoa tamko la kuitaka Serikali isitishe mchakato wa Mahakama ya Kadhi kwa kuondoa muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali namba 02 wa mwaka 2014 unaopendekeza.

Pia waliitaka serikali pamoja na mambo mengine, kufanya marekebisho kwenye Sheria ya Tamko la Sheria ya Kiislamu, Sura ya 375 (The Islamic Law (Restatement) Act, Cap.375) ambao ulitarajiwa kujadiliwa katika mkutano wa 18 wa Bunge unaoendelea Dodoma, ikiwa ni ahadi ya Serikali iliyotolewa na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda.

Baada ya tamko la maaskofu mijadala mbali mbali iliibuka huku wengine wakiwaunga mkono na wengine wakipinga kitendo chao cha kuwataka waumini wa kikristo, kushiriki mchakato huo lakini wakati wa kura ya maoni wapige kura ya hapana.

Katika mkutano wake na viongozi wa dini, jana Rais Kikwete aliainisha mambo matatu ambayo ni amani, katiba mpya na mahakama ya kadhi ambayo angependa kuyatolea ufafanuzi.

Alisema kuhusu suala la mahakama ya kadhi, uamuzi wa serikali ni kutoanzisha mahakama hiyo..
Aidha, alisema waislam hawazuiwi kuanzisha mahakama hiyo na watakapoamua kufanya hivyo serikali haitaiendesha.

KATIBA MPYA

Aliwataka viongozi wa dini kuwahimiza waumini wao kushishiriki katika mchakato wa kuupigia kura.

Alisema matamko ya baadhi ya viongozi wa dini ya kuwahimiza waumini kuikataa katiba mpya, yamemshangaza na kumsikitisha.
“Hatukutegemea viongozi wakuu kutamka hivyo licha ya haki yao ya msingi ya kutoa maoni,” alisema.

Alisema katiba iliyopo sasa inatambua hali ya kuabudu katika vifungu vya haki ya mawazo, uchaguzi wa dini na imani na kutokuwa na dini.
Askofu Mkuu wa Kanisa la Anglikana, Dayosisi ya Dar es Salaam, Dk. Valentino Mokiwa alisema kuwa, alisema watanzania wajielimishe na kuisoma katiba.

Naye, Sheikh Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Alhadi Mussa Salim, alisema viongozi wa dini wamejipanga kumaliza matatizo ya mauaji ya albino na mapambano dhidi ya dawa za kulevya.
CHANZO: NIPASHE JUMAPILI

8 comments:

Anonymous said...

Ni unafiki!!! Waislam tunakubali kwa hili wala si tatizo kuanzisha na kuendesha mahkama hizi. Tatizo kutotambuliwa mahkama hizi ndani ya sharia za nchi ni sawa na kuanzisha genge tu kwani kwa kutokubaliana hapa bado sharia za nchi hazitatowa haki kwa waislam

Anonymous said...

Huyo Rais wangu anaonyesha dhahabu za Tanzania in terms of saa na mapete!

What an ad!

Anonymous said...

KWELI NIMEAMINI KAMA TZ NI NCHI YA KIKIRISTO NA VIONGOZI WAKE WOTE WANAENDESHWA NA MAKANISA

Anonymous said...

Mdau tuelimishe haki zipi waislam hawazipati hivi sasa..ni kitu gani haswa kadhi itatoa ambacho sasa hivi hakipo. Tusaidie tusojua

Anonymous said...

Safi sana!.Hakuna sababu ya kuwa na mahakama za kidini kwa sababu tayari kuna sheria za nchi ambazo zinamlinda kila raia wa Tanzania.Hebu fikiria kila dini ianzishe mahakama yake PATAKALIKA?..

Anonymous said...

Waislaam wana mambo gani special ambayo hawaiamini sheria ya nchi??? Tanzania siyo jamhuri ya kiislaam wala haitakuwa. Sheikh mkuu wa mkoa bado anazungumzia matatizo ya dawa za kulevya na mauaji ya albino wakati serikali hii kwa mwaka wa 10 sasa imeshindwa kwa sababu haina nia ya dhati. Katiba ni mbaya na haifai kabisa kwa sababu mambo mengi yaliyopendekezwa kwa tume ya Warioba na wananchi wengi wakiwamo waislaam yameondolewa kinyemela na hiyo, vile vile katiba imepitishwa kwa mbinu chafu za chama cha Mapinduzi...KWANINI WAFANYE HIVYO? Sehemu kubwa hasa muhimu ya maadili ya uongozi yameondolewa kabisa kwa msaada wa Andrew Chenge, ina maana katiba hii itaendelea kusapoti ufisadi. WATANZANIA WENZANGU TUIKATAE KATIBA HII KWA NGUVU KWA KUWA HAINA SULUHISHO LA MATATIZO YETU, NI NAFUU ISIWEPO KATIBA KULIKO HII.

Anonymous said...

Mimi naomba kuelimishwa kidogo. Kwa nini Waislamu wanataka mahakama ya kadhi nchini Tanzania? TZ sasa ni jamhuri ya kiislamu (Islamic Republic)? Mahakama zilizopo hazitoshi? Je dini zingine zikitaka nchi ianzishe mahakama zao itakuwaje? Mimi nadhani kama suala ni kutatua migogoro kwa misingi ya kiislamu, si kuna misikiti?

Anonymous said...

Watu wote wawe na haki sawa chini ya sheria moja. Waislam tukiwa na sheria zetu tunajitengenezea nafasi ya kubaguliwa. equal rights under the law