Advertisements

Wednesday, October 22, 2014

Ufisadi wa kutisha

CAG afichua Sh. milioni 214/- zilivyolipwa waliofeli UDOM, IFM na mabilioni yanavyoliwa Tanesco
Msaidizi wa Mkaguzi Mkuu, Benja Majura

Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), inayoishia Juni 30, mwaka 2013, imeanika matumizi mabaya ya fedha za umma.

Ripoti hiyo imehusisha mashirika mengi ya umma yakiwamo Shirika la Umeme nchini (Tanesco), Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB), Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (Veta), Bodi ya Korosho, Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA), Bodi ya Pamba, mgodi wa Southern Paper Mills na Shirika la Ranchi za Taifa (Narco).

Pia, ripoti hiyo ya CAG imeeleza ukaguzi wa fedha za serikali kuu inayoonyesha fedha zilizotolewa na ambazo hazikutolewa na Hazina, Deni la Taifa, misamaha ya kodi kuwa ni asilimia kumi ya bajeti ya mwaka 2012/13 na usimamizi dhaifu wa mikataba.

Kwa mujibu wa taarifa ya CAG iliyowasilishwa jana mbele ya Kamati ya Hesabu za Serikali Kuu (PAC), na Msaidizi wa Mkaguzi Mkuu, Benja Majura, inaonyesha udhaifu mkubwa katika usimamizi wa fedha za umma kiasi cha serikali kupata hati chafu katika hesabu zake.


TANESCO
Ilionyesha kuwa Tanesco ilinunua transfoma mbili kwa gharama ya Sh. bilioni 7.879 kwa kushindanisha wazabuni 12 kwa njia ya zabuni maalum.

Alisema baada ya zoezi la awali la kuwapendekeza washindani kumalizika na kamati kuwasilisha ripoti yake, shirika liliongeza jina la kampuni ya Shadong Taikai Power Engineering, ambayo haikuwa kwenye orodha ya awali ambayo ilipitishwa na bodi ya zabuni ya shirika kuwa mshindi wa zabuni husika.

“Kampuni hiyo haikuwa na sifa, matokeo yake baada ya miezi miwili kabla ya mkataba kuisha muda wake kampuni ililiandikia shirika barua ya kutaka kubadilisha aina ya malighafi ambayo ingetumika kutengenezea transfoma kwa mujibu wa makataba hali iliyopendekeza ongezeko la kazi na bei kwa jumla ya sh. bilioni 3.707,” inaeleza taarifa hiyo.

Aidha, taarifa hiyo imeeleza kuwa Tanesco ilimlipa mkandarasi Ms Consortum Sae Power Lines and Associated Structure Ltd kiasi cha Sh. 2,876,057,520 kama fidia kwa kipindi cha miezi tisa ambacho alikaa bila kufanya kazi yeyote kutokana na mgogoro wa eneo la kupitisha mradi wa laini ya umeme katika maeneo ya Kurasini na Mbagala, Dar es Salaam.

Alisema baada ya mjadala mrefu, kampuni ya MGS International (T) Ltd ililipwa kiasi cha Sh. bilioni 1.638 na kampuni ya MPS Oil kiasi cha Sh. bilioni 1.175 kama fidia ya kuchukuliwa eneo la kupitishia mradi.

Taarifa hiyo imeanisha kuwa gharama hizo zililipwa kutokana na udhaifu wa menejimenti ya Tanesco katika kufanya upembuzi yakinifu juu ya maeneo ambayo mradi ungepita.
“Tumebaini kuwa gharama za mshauri wa mradi ziliongezeka kutoka Sh. bilioni 3.659 hadi Sh. bilioni 5.485 sawa na ongezeko la Sh. 1,825,156 bila idhini ya Bodi ya zabuni,” alibainisha.

Pia, taarifa hiyo imebainisha kuwa ukaguzi wa usimamizi wa mikataba Tanesco ulibaini kuwa lilipa gharama za ziada Sh. bilioni 9.5 kwa kampuni za Semco Martine AS na Rolls Royce Maritime AS.

“Malipo haya yalitokana na mapungufu ya menejimenti katika kufanya upembuzi yakinifu juu ya dosari za kimazingira katika mradi wa mafuta mazito, ilipelekea kufanyika uopya kwa utafiti ambao ulichelewesha mradi kwa miezi kumi na Tanesco kugharamia kiasi cha Sh. bilioni 9.5,” taarifa ya CAG inabainisha.

BODI YA MIKOPO
Taarifa hiyo imeainisha kuwa ukaguzi katika Bodi ya HESLB ulibaini kuwa mikopo ya kiasi cha Sh. milioni 214.5 kilitolewa kwa wanafunzi walioshindwa mitihani na kutoendelea na chuo na wengine waliohairisha masomo.

Taarifa hiyo imezitaja vyuo hivyo na kiwango kwenye mabano kuwa ni Algeria na Cuba (Sh. milioni 132), Chuo Kikuu cha Dodoma ( Sh. milioni 43.9), Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM) ( Sh. milioni 28.9) na Chuo Kikuu cha nchini Urusi (Sh. milioni 9.6).

SOUTHERN PAPER MILLS
Ripoti hiyo imeeleza kuwa Mgodi wa Southern Paper Mills uliuzwa kwa kampuni ya Rai Group ya Kenya kwa bei ya Sh. bilioni 1.68 wakati na thamani yake ni Sh. bilioni 43.68.

“Kwa makubaliano yaliyokuwepo, Sh. bilioni 1.68 zingelipwa wakati wa kusaini mkataba, Sh. bilioni 5.04 zingewekwa kwenye akaunti ya Escrow ambazo mwekezaji angeweza kuzitoa baada ya miaka mitatu na Sh. bilioni 37 zingewekezwa katika kipindi cha miaka mitatu, lakini baada ya uwekezaji huo mgodi umeendelea kumilikiwa na mwekezaji huyo kwa asilimia 100.

VETA
Ripoti hiyo imeonyesha kuwa Chuo cha Ufundi Mpanda kina mashine zenye thamani ya zaidi ya Sh. bilioni moja ambazo zimetelekezwa na kwamba menejimenti ya Veta ingepaswa kuweka mikakati ya kuhamisha mashine hizo ikiwa ni pamoja na kutoa mafunzo kwa walimu jinsi ya kuzitumia kulingana na utandawazi badala ya kuzitelekeza.

PRIDE, BENKI YA AZANIA
Taarifa hiyo imeeleza kuwa kwa mujibu wa taarifa za msajili wa Hazina mwaka 2008, serikali inamiliki kwa asilimia 100 ya Taasisi ya Pride Tanzania, lakini uchunguzi wa CAG ulibaini kuwa taasisi hiyo ilitolewa kwenye daftari la Msajili wa Hazina bila maelezo ya kina.

Imeeleza kuwa katika Benki ya Azania inamilikiwa kwa asilimia 91 na mifuko ya Pensheni ambayo ni Mashirika ya umma na kwamba hazijawahi kuwasilisha taarifa za hesabu kwa CAG kwa ajili ya ukaguzi.

BODI YA KOROSHO
CAG alisema ukaguzi maalum wa Bodi ya Korosho ulibaini kuwa kiasi cha Sh. bilioni 1.075 kilitumiwa na Bodi hiyo kulipia matumizi mbalimbali ya ofisi ikiwamo mishahara, gharama za matengenezo, ankara za umeme na gharama nyinginezo kinyume cha sheria inayotaka fedha hizo kutumika kwa ajili ya kuendeleza zao la korosho Mtwara.

TANTRADE
CAG amebainisha kuwa katika kipindi cha Agosti na Septemba, 2012, magari 11 yaliyosadikiwa kuwa ni ya Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara (Tantrade) yalisajiliwa kwa namba binafsi na kwamba hayakupokelewa baada ya usajili na taasisi haikujulishwa.

NARCO
Ripoti hiyo ilibainisha kuwa wafanyakazi wa Narco wamekatwa kiasi cha Sh. milioni 716.238 kwa kipindi cha Juni 1992 hadi Julai 2012, makato ya kodi na mifuko ya hifadhi ya jamii, lakini hayakupelekwa kwenye mamlaka husika kama TRA, NSSF, PPF kwa usahihi na kwa wakati.

Taarifa hiyo imeeleza kuwa Narco haikuwa na udhibiti mzuri wa fedha kwa kuwa kiasi cha Sh. milioni 392.911 hazikupelekwa benki na kutumika kwenye matumzi mengine kinyume cha sheria.

Ukaguzi huo ulibaini kuwa thamani ya ng’ombe 380 wenye thamani ya Sh. milioni 123.806 wa mradi ambao bado hawajauzwa ilikuwa ndogo ikilinganishwa na kiasi cha deni la mkopo ambao haujarejeshwa benki na kuiweka Narco katika hatari ya kuuza mali zake zilizowekwa rehani kufidia mkopo wa benki ya CRDB.

BODI YA PAMBA
CAG alisema ukaguzi ulibaini kuwa Bodi ya Pamba ina jengo la ghorofa sita, nne zinatumika na mbili hazitumiki ambazo zingeweza kuipatia kiasi cha Sh. 260,400,000 kwa mwaka.
 
CHANZO: NIPASHE

No comments: