Naibu Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, Balozi Ramadhan Mwinyi akizungumza wakati wa Mkutano wa Kamati ya Nne ya Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa iliyokuwa ikijadili ajenda kuhusu tathmini ya jumla ya Operesheni za Ulinzi wa Amani za Umoja wa Mataifa. Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni kati ya nchi zinazochangia wanajeshi wake katika operesheni hizo za ulinzi wa amani.
Sehumu ya wajumbe wa Kamati ya Nne ya Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, wakifuatilia majadiliano ya ajenda kuhusu Operesheni za Ulinzi wa Amani za Umoja wa Mataifa.
Na Mwandishi Maalum, New York
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, imeihakikishia Jumuiya ya Kimataifa ya kuwa itaendelea kushirikiana na wapenda amani katika kuisaidia Jamhuri ya Kidemokrasia
ya Kongo ( DRC) kuwa na amani na usalama.
Akichangia majadiliano
juu ya ajenda inayohusu tathimini ya jumla ya Operesheni za Ulinzi wa Amani chini ya Umoja wa Mataifa. Naibu Mwakilishi wa kudumu wa Tanzania katika
Umoja wa Mataifa, Balozi Ramadhan Mwinyi amesema, Tanzania inafanya hivyo kwa
kutambua wajibu wake katika medani ujenzi wa amani ya Kimataifa.
Amesema pia kuwa, ni kwa kutambua wajibu huo ,ndiyo
sababu iliyoifanya Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kufikia makubaliano na nchi wanachama wenzie katika SADC na Maziwa
Mkuu ( ICGLR), kujitolea kupeleka wanajeshi wake huko DRC ili kuunga mkono juhudi za kuwasaidia wananchi wa DRC kuwa na amani , usalama na maisha
yenye uhakika.
Balozi Mwinyi amesema kuwa Tanzania inajivunia kuwa wanajeshi wake
wanaohudumu kupitia FIB ambayo ni sehemu ya MONUSCO licha ya
mazingira magumu na hatari wanayokabiliana nayo wameonyesha umahiri
mkubwa ikiwa ni pamoja na kujitoa
muhanga maisha yao kuwalinda raia wasiokuwa na hatia DRC pamoja na kurejesha amani na usalama.
Kwa sababu hiyo, Naibu
Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania, amesema ni vema na haki , kujitoa
muhanga huko kwa wanajeshi
wanaohudumu FIB kutambuliwa na
wapenda amani wote na vile vile FIB iendelee kupata uungwaji mkono stahili.
Aidha Balozi Mwinyi
amesema, kutokana mabadiliko ya
mwenendo mzima wa machafuko na vita
katika maeneo mbalimbali Barani
Afrika, ikiwa ni pamoja na matishio na kutumika kwa mbinu za kigaidi na mabomu ya kutengenezwa kienyeji kunalazimisha kufanyika mabadiliko katika mfumo mzima wa ulinzi wa Amani.
Amesema, mabadiliko
hayo yanapelekea Umoja wa Mataifa kulazimika kuidhinisha matumizi ya mamlaka nguvu katika baadhi ya misheni zake kutokana na ukweli kwamba matishio hayo siyo tu ni hatari kwa raia lakini pia yamekuwa tishio kwa walinzi wa amani.
Kwa sababu hiyo, Tanzania imetaka kuwapo kwa majadiliano ya kina ndani ya Umoja wa Mataifa kuhusu dhana nzima ya mabadiliko ya mwenendo wa machafuko
na vita vinavyoendelea na hatari
inayowakabili walinzi wa amani pamoja na matumizi ya nguvu kuwa sehemu ya mamlaka nguvu ya misheni nyingi.
“ Tunahitaji majadiliano ya kina katika eneo hili, kwa sababu, mwenendo wa machafuko na mbinu za maaduzi zimebadilika kabisa. Kuna matumizi makubwa ya mbinu za kigaidi na mabomu yanayotengenezwa kienyeji, haya yote na
mengine mengi yanabadilisha kabisa historia
ya asili ya ulinzi wa amani”, amesisitiza
Balozi Mwinyi.
Vile vile amesema,
majadiliano ya kina yanahitajika katika eneo la matumizi ya teknolojia
za kisasa katika operesheni za kulinda amani,
zikiwamo ndege za kiuchunguzi zisizoendeshwa na
binadamu ( UAS).
Amesema hapana shaka, kama walivyozungumza wajumbe wengine, matumizi ya teknolojia hizo pamoja na umuhimu wake
yanahitaji majadiliano ya kina na makubaliano ya pamoja.
Aidha Balozi Mwinyi
amesema , Tanzania inakaribisha nia ya Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa ya
kufanya mapitio ya Operesheni za
Ulinzi wa Amani za Umoja wa Mataifa (
UNPKOs) na Misheni
Maalumu za Kisiasa( SPMs). Na ameahidi
kuwa Tanzania itashiriki
kikamilifu katika mchakato huo.
Awali akizugumza
mwanzoni mwa majadiliano hayo Mkuu wa Idara ya Operesheni ya Kulinda Amani ya Umoja wa Mataifa ( DPKO) Bw.
Herve Ladsous, amezungumzia mafanikio na
changamoto mbalimbali zinazokabili
shughuli za ulinzi wa amani.
Amesema katika DRC, Misheni ya Kulinda Amani ( MONUSCO)
ambayo ndani yake kuna FIB imeonyesha
umahiri na ujasiri mkubwa wa kutokubali
kurudi nyuma katika mapambano yake dhidi ya makundi ya waasi yenye silaha.
Akasema uchupavu na uhodari huo, licha ya kutoa ulinzi kwa
raia pia umefungua fursa mpya ambapo mamlaka za kiutawala za DRC zimeweza
kutawala maeneo ambayo huko nyuma yalikuwa yakishikiliwa na kukaliwa na makundi
ya waasi.
Katika majadiliano
hayo wazumgumzaji wengi wameelezea kusikitishwa kwao na ongezeko la vitendo vya kuvamiwa kwa walinzi
wa amani na kusababisha wengi wao
kupoteza maisha.
Wakasema, jambo hilo
halikubaliki na halipashwi kuendelea kufumbiwa
macho na kwamba ni j lazima pafanyike utafiti wa kina wa kwanini kumekuwa na ongezeko la
mashambulizi kwa walinzi wa amani . na wametaka
wahusika wa hujuma hizo watafutwe
na kufikishwa mbele ya vyombo vya sheria.
Wachangiaji wengine wameshauri na kutoa wito kwa
Umoja wa Mataifa kupitia DPKO na taasisi nyingine zinazohusika na
masuala ya operesheni za ulinzi wa
amani, kuangalia upya mazingira ya
utendaji kazi ya walinzi hao wa amani,
ikiwa ni pamoja na kuwapatia mafunzo zaidi yanayoendana na wakati, vifaa na zana za
kisasa na vya uhakika, malipo stahili na pia mamlaka
zinazotekelezeka.
No comments:
Post a Comment